Thursday, September 4, 2014

MAKUTANO YA TAI na JAMES KALEKWA.

By Jimmy  |  9:17 AM No comments

 Ongoza kimkakati
 
Wafilipi 3:12
"Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwaajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu."
2Timotheo 4:6
"Kwa maana,mimi sasa namiminwa,na wakati wa kufariki kwangu umefika.Nimevipiga vita vilivyo vizuri,mwendo nimeumaliza,
Imani nimeilinda;baada ya hayo nimewekewa taji ya haki,ambayo Bwana mhukumu wa haki,atanipa siku ile;wala si mimi tu,bali na watu wote waliopenda kufunuliwa kwake."

Huwezi kusema umefika au la iwapo hujui unakwenda wapi, vilevile huwezi kukaza mwendo kuelekea kule usikokujua.  “Kuna umuhimu gani wa kupiga mbio, iwapo hauko katika njia sahihi?"
Kuna kitu kinachomfanya Mtume Paulo awaandikie Wafilipi kwamba bado hajafika na anakaza mwendo na anamwandikia Timotheo, mwanae katika imani tuliyonayo kwamba mwendo ameumaliza kwa tafsiri nyingine ni kwamba hakazi tena mwendo; na kitu hicho ni malengo.

 Je, wajua???.... Malengo hukamilishwa kwa mikakati.

Sifa kubwa ya malengo ni kuzaa msukumo ndani mwa yule ayabebae wa kuyatekeleza. Kama malengo hayakusukumi kuanza utendaji, bado hayajawa malengo. Hii ni kwasababu malengo hayajikamilishi menyewe bali hukamilishwa kwa mikakati.
Mkakati ni mbinu, hatua madhubuti, wajibu, jukumu… ni utendaji/utembeaji kuelekea kwenye malengo husika. Kwa ujumla wake, mkakati ni mchanganuo wa wajibu/majukumu, wahusika, muda wa utekelezaji na rasilimali zinazohitajika kwaajili ya kukamilisha lengo fulani.


Luka 14:18
"Maana ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumaliza?"
Bwana Yesu anatutambulisha kwenye wazo moja la msingi sana ambalo tunapaswa kujifunza kwalo kwa moyo na nguvu zetu zote. Anazungumza kwa lugha ya kawaida sana kwa kutumia mfano wa Ujenzi… Hakuna mtu anayeanza shughuli ya Ujenzi bila kukaa chini na kuhesabu gharama na kuona kama anavyo vya kuumaliza! Yesu anaposema “kuhesabu gharama.” Anamaanisha si tu fedha kama ambavyo wengi hudhani moja kwa moja… Unaweza kuwa na fedha lakini huna muda, watu, nguvu kazi, nafasi n.k kwahiyo lazima tuelekeze akili zetu kumuelewa Yesu kwa kina na mapana.
Je, unavyo vya kutosha kukamilisha malengo yako? Jibu la swali huli huzaliwa kwa jinsi ambavyo utatumia muda kufanya uchambuzi na kutengeneza mkakati.
Kuna watu wengi sana nimewashuhudia na marafiki zangu kadhaa wamenaswa kwenye mkwamo ambao hata mimi hapo awali nilijikuta nimekwama na hata sasa ninajuhudi za kupigana vita kepuka mkwamo huo… kuanza jambo na kutolikamilisha! Mkakati unakusaidia kujinasua kutoka kwenye mkwamo huo. Ninaomba uambatane nami kuchanganua mambo muhimu ndani ya mkakati.
        i.            Wajibu/Jukumu – Huu ni mchanganuo wa kazi ndogo ndogo ili kulielekea lengo husika.

     ii.            Wahusika – Ndani ya mkakati unapaswa kuainisha nani atahusika kufanya nini. Ni muhimu sana mkakati ufikie hatua ya kugawa majukumu na wajibu kwa muhusika fulani kwaajili ya utendaji. Kutokana na aina ya malengo, vyaweza kuwepo vigezo vya kumbebesha mtu fulani wajibu au jukumu: mfano upatikanaji wake, kipaji, uwezo, uzoefu, ujuzi n.k

   iii.            Muda/Wakati – Hii ni rasilimali muhimu amabayo kila mtu amepewa sawasawa. Kila mtu ana masaa ishirini na nne  (24) ndani ya siku moja, siku saba ndani ya wiki moja. Kinachojenga tofauti miongoni mwetu ni namna tunatumia muda wetu. Ni LAZIMA ufanye maamuzi ni muda kiasi gani utahitajika kwaajili ya kuleta utimilifu wa jukumu fulani. Usidhani utafanya jambo moja muda wote! Kwahiyo, ni lazima kwa mfano kusema “Nitaandaa rasimu ya mafundisho/kitabu ndani ya wiki ya kwanza ya mwezi wa pili yaani tarehe 1- 7 Februari.” Au unaweza kutumia Mchanganuo wa jedwali kama nilivyofundisha hapo awali na nitaweka mfano huo tena baada ya Maelezo haya juu ya mkakati. Usipochanganua muda hiyo ni dalili ya kuanza kutumia vibaya muda wako, utaanza kufanya chochote wakati wowote… jukumu la tisa utaanza nalo, utajikuta unatamani kufanya jukumu la nne, mara unaona jukumu la saba linaibuka likifuatiwa na jukumu la kwanza… Hutakuwa na mtiririko maalum! Kwahiyo utajikuta katika ya mwaka hujafanya chochote cha maana zaidi ya kurukaruka tu huku na kule.

   iv.            Rasilimali fedha –Masikioni mwa watu wengi sana ukisema rasilimali, huja Taswira ya fedha. Lakini kwangu binafsi hii huja kama rasilimali ya mwisho… Kwa mfano, unadhani unahitaji fedha kiasi gani kuandika kitabu??? Hauhitaji hata senti moja kuandika kitabu ila kuchapisha kitabu ndiyo unahitaji pesa… Sasa,  ni hekima sana kujua ya kwamba kabla ya kitabu kuchapishwa, kwanza huandikwa! Kwahiyo, usisingizie fedha… Kaa chini uandike. Anza kufanya yaliyo ndani ya uwezo wako kwanza. Mkakati mzuri ni ule ambao hukusukuma kufanya Mchanganuo wa rasilimali fedha. Hii hupelekea kujua ni fedha kiasi gani zitahitajika ili kukamilisha jukumu fulani. Lakini zaidi ya hapo ni lazima kujua kiasi hicho cha fedha kitahitajika kwa wakati gani. Vilevile, ni muhimu kuainisha vyanzo vyako vya mapato (jinsi gani fedha hiyo itapatikana) – mshahara, faida ya biashara, gawio, mkopo, changizo (harambee), ufadhili n.k hii itakusaidia sana kutembea kwa Uhakika na kutoshangazwa na mambo mengi (not to be caught by surprise).

      v.            Nguvu kazi – huu ni uwezo ulifichika ndani ya mtu (hazina). Uwezo huu huyaleta mawazo katika uhalisia… Husababisha vitu kuwa halisi. Ni mjumuisho wa ujuzi, Uzoefu, ufahamu na nguvu. Kwa mfano, ili uwe na kitabu au mafundisho kama haya ni lazima uandishi, mitindo ya uandishi na utumuzi wa lugha viingie kazini. Lazima kalamu na karatasi au ipad, kompyuta mpakato n.k vitumiwe na mtu ili kuzalisha matokeo. Ile Akili, fikra na mawazo ndiyo nguvu kazi. Lazima mkakati wako ukusukume kutambua na kuyachambua haya kinagaubaga.
Kumbuka, unafanya uchambuzi wote huo kwa lengo kuu la kujibu swali Je, unavyo vya kutosha kukamilisha ujenzi wa mnara?

 

Author: Jimmy

Hello, I am Author, decode to know more: In commodo magna nisl, ac porta turpis blandit quis. Lorem ipsum dolor sit amet, consectetur adipiscing elit. In commodo magna nisl, ac porta turpis blandit quis. Lorem ipsum dolor sit amet.

0 comments:

E-mail Newsletter

Sign up now to receive breaking news and to hear what's new with us.

Recent Articles

© 2014 Uncle Jimmy | Distributed By My Blogger Themes | Created By BloggerTheme9
TOP